Simba yamfaidi refa mechi yao na Yanga

MWAMUZI ambaye Yanga wana bifu naye, Martin Saanya amekabidhiwa kuchezesha mechi ya watani wa jadi Jumapili ijayo, Mwanaspoti limethibitisha. Mwamuzi huyo mwaka 2009 alikuwa wa akiba wakati Yanga ilipotoka sare na Simba lakini mwaka 2013 Simba ilipolala mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Taifa ndiye aliyechezesha.
Hata hivyo, aliingia kwenye mzozo na Yanga baada ya kutoa penalti kwa Coastal Union kwenye dakika za lala salama na mechi kumalizika kwa sare ya bao 1-1 kwenye msimu wa 2012/13, jambo ambalo liliifanya Yanga kumchukia na kukosa imani naye.
Saanya ambaye alifungiwa na Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) mwaka mzima kwa kushindwa kumudu mechi hiyo ambayo ilisababisha mashabiki wa Yanga kuharibu mali za Uwanja wa Mkwakwani pamoja na basi la Coastal Union.
Kabla ya mchezo huo, mwamuzi huyo alikuwa akituhumiwa na mashabiki wa Yanga kwamba aliibeba Simba kwenye mechi ya hisani dhidi ya Azam. Simba ilishinda mabao 3-2 huku Azam wakidai kunyimwa penalti mbili za wazi.
Habari kutoka ndani ya TFF zimedai kuwa mwamuzi huyo mwenye beji ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), ndiye atakayeamua nani mbabe katika mechi hiyo ambayo itashuhudia Kocha Mserbia, Goran Kopunovic akiiongoza Simba kwa mara ya kwanza kwenye mechi ya watani wa jadi nchini.
Tayari Simba wametimka Jiji la Dar es Salaam na kwenda visiwani Unguja ambako mara nyingi wanaamini wakitokea huko hupata matokeo mazuri kutokana na utulivu wa mazingira ambao unawafanya akili zao zitulie katika jambo moja tu.
Saanya amewahi kuichezesha mechi ya Simba na Yanga mara moja msimu wa 20012/13 kabla ya kufungiwa na matokeo ya mechi  hiyo ilikuwa ni sare ya bao 1-1. Simba ilianza vibaya ligi hiyo na ilijikongoja na kupanda mpaka nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 23 na itaingia uwanjani ikitoka kuifunga Prisons mabao 5-0 wakati Yanga yenyewe inaongoza ligi ikiwa na pointi 31 na tayari imefuzu hatua ya pili kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika kwa kuitoa BDF XI ya Botswana na sasa itakutana na Platinum ya nchini Zimbabwe.
Share on Google Plus

About ahmed

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment