KIKWETE USO KWA USO NA UKAWA


Dodoma/Dar. Wakati wowote wiki hii, Rais Jakaya Kikwete anatarajia kukutana na viongozi wa Vyama vya Siasa vinavyounda Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) ili kuzungumzia mchakato wa Katiba.
Katika mkutano huo, Rais Kikwete atakutaka ‘kiaina’ na wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ambao unaundwa na vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema na CUF.
Aprili 16, mwaka huu wajumbe wa Ukawa na baadhi kutoka Kundi la 201, walisusia vikao vya Bunge hilo wakitaka msingi wa mapendekezo ya Rasimu ya Katiba usibadilishwe, wakipinga uamuzi wa CCM kutaka kuingiza mfumo wa serikali mbili badala ya tatu zilizopendekezwa katika Rasimu.
TCD inaundwa na vyama vya siasa vyenye uwakilishi bungeni ambavyo ni CCM, CUF, Chadema, NCCR-Mageuzi, UDP na TLP, huku vyama visivyo na uwakilishi bungeni vikiwakilishwa na UPDP kinachoongozwa na Fahmi Dovutwa.
Jana, kwa nyakati tofauti wenyeviti wenza wa Ukawa, Freeman Mbowe (Chadema) na Profesa Ibrahim Lipumba (CUF) na James Mbatia (NCCR Mageuzi), walisema wako tayari kukutana na Rais, ila msimamo wao wa kutaka ijadiliwe rasimu iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Kimekuwa ni kilio cha muda mrefu kwa Ukawa kuomba wakutane na Rais Kikwete kwa ajili ya kujadiliana namna bora ya kuendesha mchakato wa kupata Katiba Mpya.
Akizungumza na waandishi wa habari bungeni Dodoma jana, Mwenyekiti wa TCD, John Cheyo alisema Rais atafanya kikao hicho wakati wowote ndani ya wiki hii na kwamba viongozi wa vyama wakiwamo wa Ukawa, wamethibitisha kushiriki.
Cheyo alisema, katika kikao walichokutana Dar es Salaam Agosti 23, wanachama wa TCD walikubaliana kwamba upo umuhimu wa kukutana na Rais Kikwete kwa mazungumzo na maridhiano.
Kukutana kwa viongozi hao, kunakuja huku wajumbe wa Bunge Maalumu wakiwa wamemaliza kujadili sura zote 15 zilizokuwa zimesalia na tayari baadhi ya kamati zimemaliza kupiga kura wakisubiri kuingia bungeni Septemba 2 kwa kazi ya kupigia kura sura kwa sura.
Kuhusu viongozi wa Ukawa, alisema wanazo taarifa na baadhi yao walikuwapo katika kikao cha kujadili kukutana na kiongozi huyo wa nchi, hivyo akasema lazima watashiriki wakati wowote wakiitwa.
Lipumba
Akizungumzia mkutano huo na Rais, Profesa Lipumba alisema: “Tunakutana na Rais Kikwete kwa sababu sisi ni wanachama wa TCD.” Alipoulizwa juu ya msimamo wa Ukawa, alisema lengo ni kutafuta mwafaka ili mchakato wa kupata Katiba Mpya uendeshwe kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu.
Share on Google Plus

About ahmed

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment