NUHU, SHILOLE YANAKUJAJE KIZAZI HIKI?

BAHATI mbaya sana, simjui huyu bwana mdogo, anayekwenda kwa jina la Nuhu Mziwanda, aliyekuwa rafiki wa kiume wa msanii anayekimbiza katika muziki wa mduara, Zuwena Mohamed maarufu kama Shilole.
Naambiwa naye ni msanii wa muziki wa kizazi kipya, ingawa sijawahi kuisikia kazi yake yoyote. Lakini nikiri kuwa nimeiona picha yake mara nyingi, akiwa na mpenziwe na hata na watu wengine. Ni kijana mtanashati anayeweza kuwavutia wasichana wanaopenda mabrazamen!
Kwa muda mrefu, Nuhu na Shilole walikuwa wakiishi pamoja kama mtu na mpenzi wake. Mara kadhaa, yamewahi kuibuka madai kuwa kijana huyo alikuwa ni mdogo kiumri kwa msichana, lakini mara zote, mkali huyo wa kibao cha Paka la Baa amekuwa akikataa.
Binafsi aliwahi kuniambia wanaosema umri mdogo wa mpenzi wake, ni wambeya, wanamuonea wivu, kwa sababu yeye ana umri sawa na mwenzake. Haina ubishi kwamba walipendana na ili kuwathibitishia watu hivyo, Nuhu alijichora tatoo kwenye paja la mkono wake, akiwa ameandika maandishi yanayosomeka Shishi Baby, jina lingine la kisanii la Shilole!
Lakini katika hali isiyotarajiwa, penzi la Shilole na Nuhu likaparanganyika ghafla. Ni hapa ndipo ninapotaka kujikita leo ninapozungumza na huyu bwana mdogo. Najua, umri wake bado mdogo, hivyo kuna mambo mengi kwake ni mageni na asiyo na uzoefu nayo.
Kwa mujibu wa mashuhuda, tatoo aliyojichora Nuhu, ni ile ambayo haiwezi kufutika, kwa maana hiyo pamoja na kupigwa kibuti, Shishi Baby itaendelea kung’ara mkononi mwake na kila siku ataiona.
Moja kati ya vitu ambavyo mtu anapaswa kuviogopa na kuwa na tahadhari kubwa kabisa ni mapenzi, hasa haya ya kizazi cha sasa chenye kupenda kuiga, anasa, utanashati na kulelewa (Shugamami na shugadadi).
Mapenzi yamesababisha wengi kuharibu maisha yao na kama mnavyojua, watu wanauana kila siku, mke au mume anamuua mwenzake, tena wakati mwingine, kikatili kabisa. Mapenzi ya siku hizi yanahitaji ‘timing’. Uaminifu, siyo tu ule wa kutotoka nje ya ndoa, bali kupendana kwa dhati ya moyo, haupo.
Watu wanapendana kulingana na upepo unavyokwenda, leo wanashibana sana, kesho chui na paka.
Hatukatai kuonyeshana mapenzi, tunawaona watu ufukweni kila siku wameshikana viuno, wanakulana denda hadharani na wakati mwingine hata zaidi ya hapo. Ni wakati wao, unaruhusu kwa sababu ni nyakati za furaha. Kesho wakigombana, kukumbatiana kwao jana ufukweni hakuonekani.
Kwanza, utamaduni wa kujichora tatoo binafsi huwa siupendi kwa vile naamini siyo wetu, ni wa kuiga. Lakini kama ni kuongeza mapambo mwilini kwa kuwa wao ni wasanii, zipo tatoo za kujichora kwa rangi, badala ya hizi za kutoboa mwili. Siku ikikuchosha, unaitoa.
Halafu, nadhani kama ni kujichora kuonyesha mapenzi kwa mtu, watu pekee wenye hadhi hiyo ni watoto wako, mama au baba yako. Hawa, vyovyote itakavyokuwa, hata mgombane vipi, bado watabaki kuwa ni damu yako.
Nasisitiza tena, kila mtu ana haki ya kupenda atakavyo, lakini jambo moja muhimu ambalo nina uzoefu nalo, mapenzi ya enzi hizi za dotcom ni ya upepo. Kuna machungu mengi ambayo yanawafanya watu kujutia uamuzi wao wa kuoa au kuolewa na walionao sasa. Wakati mababu zetu walizeekea kwenye ndoa, asilimia chache sana ya vijana wa sasa wanaoweza, angalau kukaa miaka kumi katika ndoa.
Sidhani kama kweli Nuhu alimpenda kihivyo Shilole na kama ndivyo, nimpe pole na kumtahadharisha asije chora tena tatoo nyingine ya mwanamke mwilini mwake, wanaume wenzake watamcheka!
Share on Google Plus

About ahmed

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment