BAADA ya kuikung’uta Yanga na kusogea mpaka nafasi ya tatu
kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara, matajiri wa Simba wamekaa mezani na
kuanza kupiga hesabu za Azam na Yanga huku wakikomaa kuhakikisha Mnyama
hatelezi wala hadondoshi pointi hata moja katika mechi nane zilizobaki
kumaliza msimu.
Simba imeanza dua mbaya kuhakikisha kwamba Yanga
na Azam zinapoteza uelekeo angalau kwenye mechi tatu mpaka nne ili wao
wakishinda wakae pazuri na kujihakikishia wanakwea Pipa mwakani kurejea
kwenye michuano ya kimataifa.
Simba ilikuwa na mwendo wa kusuasua mwanzoni mwa
msimu huu na kushika nafasi za chini kwenye msimamo, lakini ushindi
walioupata dhidi ya Yanga Jumapili wa bao 1-0 umeifanya timu hiyo
kufikisha pointi 26 na kufanya tofauti yao na Yanga wanaoongoza ligi
kuwa pointi tano tu.
Vijana hao wa Mserbia Goran Kopunovic sasa
wanatakiwa kuhakikisha wanapata ushindi katika mechi zao nane za mwisho
ikiwemo dhidi ya Azam FC ili kuweza kupunguza tofauti yao ya pointi na
vinara wa ligi.
Simba ambayo iko chini ya viongozi wanaosifika kwa
utajiri ikishinda mechi hizo itamaliza ligi na pointi 50 ambazo kama
Yanga na Azam watapoteza mechi mbili na kupata sare michezo mingine
hawataweza kuzifikia. Azam wakishinda mechi zao tisa zilizobaki
watafikisha pointi 57 huku Yanga ambayo ina idadi ya mechi sawa na Azam
ikikomea pointi 58 ambazo hazitakuwa na faida yoyote kwa Simba kwani
itaondolewa kwenye nafasi mbili za juu.
Simba ikishinda mchezo wake na Azam itakuwa
imefanya tofauti yao ya pointi na mabingwa hao watetezi wa ligi kuwa
moja hivyo kujiweka katika nafasi nzuri ya kuichungulia michuano hiyo ya
Afrika ambayo hawajashiriki kwa miaka miwili sasa.
Kocha Kopunovic alisema mechi yao na Azam ni
muhimu, pia alisisitiza kuwa hatazami tofauti yao ya pointi na Azam wala
Yanga bali anatazama mechi zilizoko mbele yake na kuhakikisha timu yake
inapata ushindi katika michezo yote hiyo. “Ni kweli tuna mechi dhidi ya
Azam ambayo ni muhimu, nazitazama pia mechi nyingine zote na
kuhakikisha tunashinda zote ili mwisho wa msimu tupige hesabu tumemaliza
katika nafasi gani,” alisema Kopunovic.
0 comments:
Post a Comment