Simba yazitesa Yanga, Azam FC

BAADA ya kuikung’uta Yanga na kusogea mpaka nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara, matajiri wa Simba wamekaa mezani na kuanza kupiga hesabu za Azam na Yanga huku wakikomaa kuhakikisha Mnyama hatelezi wala hadondoshi pointi hata moja katika mechi nane zilizobaki kumaliza msimu.
Simba imeanza dua mbaya kuhakikisha kwamba Yanga na Azam zinapoteza uelekeo angalau kwenye mechi tatu mpaka nne ili wao wakishinda wakae pazuri na kujihakikishia wanakwea Pipa mwakani kurejea kwenye michuano ya kimataifa.
Simba ilikuwa na mwendo wa kusuasua mwanzoni mwa msimu huu na kushika nafasi za chini kwenye msimamo, lakini ushindi walioupata dhidi ya Yanga Jumapili wa bao 1-0 umeifanya timu hiyo kufikisha pointi 26 na kufanya tofauti yao na Yanga wanaoongoza ligi kuwa pointi tano tu.
Vijana hao wa Mserbia Goran Kopunovic sasa wanatakiwa kuhakikisha wanapata ushindi katika mechi zao nane za mwisho ikiwemo dhidi ya Azam FC ili kuweza kupunguza tofauti yao ya pointi na vinara wa ligi.
Simba ambayo iko chini ya viongozi wanaosifika kwa utajiri ikishinda mechi hizo itamaliza ligi na pointi 50 ambazo kama Yanga na Azam watapoteza mechi mbili na kupata sare michezo mingine hawataweza kuzifikia. Azam wakishinda mechi zao tisa zilizobaki watafikisha pointi 57 huku Yanga ambayo ina idadi ya mechi sawa na Azam ikikomea pointi 58 ambazo hazitakuwa na faida yoyote kwa Simba kwani itaondolewa kwenye nafasi mbili za juu.
Simba ikishinda mchezo wake na Azam itakuwa imefanya tofauti yao ya pointi na mabingwa hao watetezi wa ligi kuwa moja hivyo kujiweka katika nafasi nzuri ya kuichungulia michuano hiyo ya Afrika ambayo hawajashiriki kwa miaka miwili sasa.
Kocha Kopunovic alisema mechi yao na Azam ni muhimu, pia alisisitiza kuwa hatazami tofauti yao ya pointi na Azam wala Yanga bali anatazama mechi zilizoko mbele yake na kuhakikisha timu yake inapata ushindi katika michezo yote hiyo. “Ni kweli tuna mechi dhidi ya Azam ambayo ni muhimu, nazitazama pia mechi nyingine zote na kuhakikisha tunashinda zote ili mwisho wa msimu tupige hesabu tumemaliza katika nafasi gani,” alisema Kopunovic.
Share on Google Plus

About ahmed

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment