WIZARA YA AFYA UJUMBE WA EZRA MMEUCHUKULIAJE?

Kaimu Katibu mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Bi. Regina Kikuli.
NUKUU ya kusikitisha aliyoiacha mwanafunzi Ezra Gerald Wabamba aliyejinyonga katika Hospitali ya Mkoa wa Kagera ilisomeka hivi:  “Haiwezekani binadamu kuhudumiwa kama mbwa, yaani nafika hospitali naeleza hali yangu halafu daktari ananiandikia kulazwa bila ya kupimwa, sasa sijui watatibu  nini?
“Kwa kweli siwezi kuvumilia yaani wenzangu wanasoma halafu mimi nimekalishwa tu hapa hospitalini bila ya kujua wananitibu nini, inaniuma sana  mpaka kufika hatua hii ya kujiondoa duniani, ni kwa sababu ninaona wanachezea ndoto zangu, mimi siwezi kuona ndoto yangu inazimwa wakati ninatakiwa niwepo shuleni nikamilishe ndoto zangu, mjitahidi tukutane mbinguni.”
Kwa mtu mwenye kujali ujumbe huu ni mzito sana, hauwezi kupuuzwa kwa namna yoyote kwa sababu una msingi wa malalamiko ya kila siku juu ya matibabu katika hospitali zetu nchini. Kwa wanaoacha upepo wake upite wanaweza wasione madhara, lakini dunia imeshuhudia hivi karibuni serikali ya Tunisia ikiangushwa madarakani kwa sababu ya muuza matunda.
Mchuuzi huyo wa matunda aitwaye Mohammed Boaziz hakuonekana kuwa tishio katika utawala wa Rais Ben- Ali wa nchi hiyo, kama ambavyo kifo cha Ezra kinavyoweza kuchukuliwa.
Tafsiri inayowafanya  wakuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ni: “Mtoto mwenyewe ni mwanafunzi tena anatoka katika familia maskini ambayo haiwezi kufanya chochote cha kudhuru nafasi zetu za uongozi.”
Kasumba hii ndiyo aliyokuwa nayo Ben Ali na wasaidizi wake, aliwachukulia watu maskini kama vikaragosi ambao hawawezi kuwa na madhara katika utawala wake, dola iliwaonea itakavyo, machozi ya walalahoi yalichukuliwa sawa na ya samaki kuishia baharini lakini kauli ya Ezra ya ‘tukutane mbinguni’ ina maana kubwa sana.
Wengi huamini mbinguni ndiko kuliko na haki, imani ambayo Boaziz wakati akijilipua kwa petro aliamini pia kuwa bora atangulie kwa mtoa haki ili waliomtesa watakapokwenda huko wahukumiwe kwa dhuluma zao.
Lakini wakati imani hiyo inaheshimiwa hasa na wenye dini, kuna baadhi husema malipo ya haki hulipwa hapahapa duniani, naamini hivyo kwa ushahidi uliotokea Tunisia.Kinachoniogopesha ni mkondo huo kuikumba nchi yangu pia. Maana yaliyokuwa yakifanywa na watawala wa nchi hiyo yameanza kufanyika hapa, haki ya raia haipatikani kirahisi. Malalamiko yaliyomuondoa Ezra duniani siyo mageni, serikali inajua kuwa hospitali zake nyingi huduma zimezorota kwa kiwango kikubwa. Wagonjwa wanalazwa bila kupewa huduma stahili.
Nilidhani tukio la kifo cha Ezra lingechukuliwa kama mwanzo wa safari ya wizara kujisafisha, lakini wasemaji wake waliniambia kuwa tukio hilo hawawezi kulizungumzia kwa sasa kwa sababu limeshakuwa jinai.
Hilo halizungumziki kwa sababu hiyo, je malalamiko mengine ambayo yanatolewana na wagonjwa juu ya kukosekana kwa dawa hata za kutuliza maumivu kwenye hospitali nyingi za serikali ikiwemo ya Palestina, Mwananyamala zilizopo jijini Dar es Salaam na karibu hospitali nyingi za mikoa hali ya matibabu haziridhishi hata kidogo, vipi hiyo nayo ni jinai isiyozungumzika?
Ushauri wangu kwa serikali, pamoja na kukipuuza kifo cha mwanafunzi huyo kama ukimya unavyoendelea hivi sasa, desturi hii ya kutokujali vilio vya wanachi iachwe kwa sababu kadiri siku zinavyokwenda wafuasi wa kupigania haki zao wanaongezeka. Leo mtawazima kwa mabomu na risasi za moto lakini Tunisia walishindwa kuwatuliza kwa ndege za kivita na vifaru.
Mwisho Wizara ya Afya ifuatilie kwa ukaribu tukio la kifo cha Ezra na kutoa ripoti ambayo itawaacha huru wananchi kutoka kwenye hisia za vilio vyao kupuuzwa na kuamini kuwa serikali yao inawajali. Nachochea tu!
Share on Google Plus

About ahmed

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment