Israeli yaua makamanda 3 wa Hamas.

Pengo lililowachwa na jengo la orofa nne lililoharibiwa kabisa katika shambulizi hilo
Shambulizi la Israeli kwenye nyumba moja mjini Rafa limewauwa makamanda watatu wakuu katika jeshi la Hamas.
Huduma za uokoaji za Palestina zinasema kwamba watatu hao Mohammed Abu Shamala, Mohammed Barhoum and Raed al-Attar waliuawa karibu na mji wa kusini wa Rafah miongoni mwa watu sita waliouawa.
Mashambulizi yalianza upya siku ya jumanne kila upande ukilaumu mwengine kwa kutofaulu kwa mazungumzo ya amani mjini Cairo huku Israeli ikiapa kuendelea na kampeni hadi usalama wake uimarike.
Mwandishi wa BBC Yolande Knell anaripoti kwamba makamanda hao watatu walikuwa nguzo kuu ya kwa operesheni zinazohusisha kupenyeza, ujenzi wa handaki na kumteka mwanajeshi wa Israeli, Gilad Shalit.
Babu ya watoto watatu waliouawa Gaza akiomboleza Gaza
Bwana Attar alikuwa kamanda mkuu zaidi katika eneo la kusini na alionekana akimpeleka Bwana Shalit kutoka kwa gari na kumpatiana kwa Wamisri wakati wa mabadilisho ya mfungwa mwaka wa 2011.
Bwana Shamala alikuwa kamanda wa Rafah aliyesemekana kuwa na jukumu la kupanga kutekwa kwa Shalit.
Bwana Barhoum naye ambaye ni jamaa wa karibu wa Fawzi Barhoum msemaji wa Hamas alikuwa kamanda mkuu wa mitaa.
Katika maendeleo mengine, Hamas imeonya kampuni za ndege za nchi za kigeni kusimamisha safari zake za ndege kwenda na kutoka katika uwanja wa ndege wa Gurion mjini Tel Aviv kuanza Alhamisi.
Usalama umeimarishwa katika uwanja wa Ndege wa Ben Gurion
Kundi hilo pia limehakikisha kwamba litaacha kutia juhudi za mazungumzo ya kusitisha mapigano kabisa nchini Israeli.
Baraza la usalama la umoja wa mataifa limeeleza wasiwasi wake kutokana na kurejea kwa uadui na likaitaka pande hizo mbili kurejelea meza ya mazungumzo.
UN inahimiza kupatikana suluhisho la kudumu haraka iwezekanavyo ili kusitisha mapigano hayo.
Misri pia imeeleza masikitiko makubwa baada ya siku kumi za mazungumzo ya amani na ikasema kwamba itaendelea kutafuta suluhisho la kudumu.
Share on Google Plus

About ahmed

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment